Kama tunataka kwenda ‘Sauzi’ 2010

April 7, 2008

KATIKA safu hii, tutakuwa tukiwaletea makala hii kila Jumatatu, itakayokuwa ikizungumzia nini kifanyike ili Tanzania, iweze kucheza fainali za Kombe la Dunia.

Kuna mambo mengi ya msingi ambayo kwayo, soka ya Tanzania itapiga hatua kubwa, ikiwamo kuwekeza katika soka ya vijana na kuongoza soka kisayansi zaidi. Kwa mfano, timu chini ya umri wa miaka 17 inapaswa kuwa chini ya kocha mkuu na timu ya umri wa miaka 15, ambao wote watapaswa kuwajibika kwa kocha mkuu wa timu ya Tanzania, Taifa Stars, Mbrazil Marcio Maximo. Nane, chini ya umri wa miaka 15 na 17 watapelekwa kwenye nchi zenye soka ya hali ya juu ili kufanya majaribio ya mechi za kimataifa na wenye umri kama huo. Wanaweza kupelekwa kama Mexico, Brazil, Argentina, Colombia, Uruguay, Paraguay, Ureno, Ufaransa, Czech, Uingereza na Ujerumani kwani soka yao iko juu. Tisa, vijana wa chini ya umri wa miaka saba baada ya kucheza mechi kadhaa za kimataifa za kirafiki za ndani na nje ya bara la Afrika, kutokana na mikakati hiyo, taifa litakuwa limeandaa timu bora na ya kudumu ambayo itakuwa ikipokezana na vijana wa chini ya umri wa miaka 15 ambao nao watakuwa wakichukua nafasi za kaka zao wanaochakaa kimpira au wanapopata nafasi za kucheza soka la kulipwa nje ya taifa lao. Kumi, ili timu hizo mbili ziweze kuwa bora na za kutisha Afrika na duniani kama ilivyokuwa Zambia miaka ya nyuma chini ya utawala wa Rais Kaunda na DRC miaka ya nyuma, timu hizo ni lazima zipate mafunzo ya makocha tofauti huko nje ya nchi chini ya kocha wao mkuu. Mfano, Brazil wapate mafunzo ya maprofesa kama Neto, Mazzei, Carlos Alberto, Didi, Manga, Lula, Vardimar de Brito wakati kwa Colombia wapate mafunzo ya Profesa Marios de Pullar ambapo huitwa kwa jina la ‘Pulla’ pamoja na baadhi ya makocha wa Yugoslavia, Uingereza, Ufaransa na nk. Kumi na moja, kwa mtindo huo taifa litakuwa likipata vijana wenye vipaji vyote aina tatu kutoka kwenye programu zote mbili muhimu, yaani kutoka programu sahihi ya sita (The 6th Soccer Development Programme), ambayo huanzia shule za ‘ukuchi’ chini ya umri wa miaka mitatu mpaka vyuo vikuu na taasisi za elimu kabla hawajaingia katika programu ya mwisho inayojulikana kama General Soccer Development Programme kwa vile programu hii huchukua muda mrefu hivyo programu ya sita, yaani programu ya kanda za kitaifa. Nchi kama Tanzania inaweza kuwa na kanda (National Zonism) tano ambazo ni Mashariki, Magharibi, Kaskazini, Kusini na Kati. Maeneo ya vipaji vya soka aina zote tatu, mfano maeneo yote yenye mito ya asili yenye kuwa na samaki wa maji baridi hutoa vipaji vya juu na vya juu zaidi kama Morogoro katika vijiji vya Ifakara, Kilombero, Mahenge, Matombo na mikoa ya Kigoma katika vijiji vya Tongwe. Mbali ya maeneo yenye mito ya asili ya samaki wa maji baridi maeneo mengine ni yanapopatikana madini ya dhahabu kwani maji ya maeneo hayo hutengeneza vipaji vikubwa pamoja na mwambao wote wa Ziwa Tanganyika kutokana na samaki kupatikana kwa wingi. Mkoa wa Rukwa maeneo ya Simba, Mto Urwila na Mto Ugalla katika Wilaya ya Mpanda. Mwanza na Musoma kutoka katika mwambao wote wa Ziwa Victoria, Songea kutoka maeneo ya Mto Ruvuma. Mbeya ni maeneo ya Wilaya ya Chunya kunakopatikana dhahabu na mwambao wote wa Mto Songwe na Ziwa Nyasa kama Kyela alikotokea marehemu Willy Mwaijibe. Mkoa wa Lindi na Mtwara ambako kuna soka la kuambukizwa ambalo kitaalamu huitwa Transmission Football kutoka nchi ya Msumbiji yenye vipaji vya juu kama ilivyo kwa nchi ya Angola. Kanda ya Kati Dodoma haina vipaji sana kama ilivyo kwa Mkoa wa Tanga, lakini pia kuna soka ya kuambukizwa (Transmission Football) kutoka katika damu ya wahamiaji waliotoka mikoa yenye vipaji vya juu kutokana na kuoana kwa makabila yaliyohamia. Ikumbukwe kwamba, duniani kuna misingi mikuu minne iliyozalisha soka kama, msingi wa kwanza ni wa kipaji (Talented Football) msingi wa pili ni wa kupandikiza (Planted Football) kupitia programu ya sita mashuleni. Mpira wa kuambukiza (Transmission Football) yaani damu ya vipaji kutoka nchi nyingine na kuingia nchi isiyokuwa na vipaji pia soka ya kuigiza (Pemitational Football). Mfano, Zambia soka iko kaskazini magharibi mwa maeneo ya Kitwe, Lwamishire, Chilirabembwe, Nchampa na mingineyo. Mipakani mwa DRC yenye vipaji vya juu kutokana na mchezaji Kalala Makukula na nyinginezo ambao wamo katika historia ya maendeleo ya soka Afrika kama ilivyo kwa Pele wa Brazil mwenye asili ya Angola na Eusebio wa Ureno mwenye asili ya Msumbiji. Historia hiyo yote inatokana na utafiti wa mwaka 1958 uliofanywa nchini Uingereza baada ya Kombe la Dunia lililofanyika nchini Sweden. Brazil imepata vipaji vyake kupitia soka ya kuambukizwa. Hii ni kutokana na watumwa wengi kutoka Bara la Afrika kupelekwa kulima miwa katika mashamba makubwa ya Wazungu, bara lenye vipaji vyote duniani. Wabrazil weupe nao wamepatikana kutokana na mchanganyiko wa Wazungu, Wahindi, Wagiriki, Wafilipino na kadhalika na ikumbukwe pia miaka ya kuanzia 1890 hadi 1974, timu ya taifa ya Brazil, iliundwa na wachezaji wengi wenye asili ya Afrika. Tukutane Jumatatu ijayo.